Skip to main content
Imechapishwa na Policy Forum

Kufuatia ugunduzi wa  uhakika wa hivi karibuni wa gesi  asilia Tanzania, nchi imejitokeza kuwa na uwezekano mkubwa wa uzalishaji gesi kwa kiwango cha juu katika Afrika ya Mashariki, na kuleta hamasa miongoni mwa  wananchi, jumuiya za kiraia, na wanasiasa kuhusu  matarajio ya  rasilimali  hiyo kuchochea maendeleo ya taifa .  Serikali,  inaaminika,  imeanza mchakato  wa kuandaa sera na miundo ya kisheria zitakazosaidia usimamizi  wa  uchunguzi, uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa gesi asilia.   Kumekuwa  na malalamishi mengi hata hivyo, kwamba siyo mengi yalifanyika kuboresha uwazi katika sera za kifedha na masharti ya mikataba ya uziduaji kwa ujumla.  

Taarifa za kuvuja hivi karibuni kwa Mkataba wa Nyongeza wa Ushirikiano katika Uzalishaji (Production Sharing Agreement -PSA)  kati ya “Statoil”,  yaani Kampuni ya Mafuta  ya Taifa la Norway na Serikali,  na utata uliozuka miongoni mwa wananchi, zinaonesha umuhimu wa utaratibu wa kuweka wazi mikataba yote inayohusu uziduaji nchini Tanzania.  

Sisi Asasi za Kiraia tajwa hapa chini, tumekuwa tukifuatilia majadiliano na maoni ya wadau mbali mbali kuhusu suala hili  kwa shauku kubwa. Kama matokeo yake, tarehe 15th ya mwezi wa  Agosti, 2014 tulijadili kuhusu chambuzi mbali mbali  kwa lengo la  kutoa maoni yetu kama asasi za kiraia na msimamo wetu kuhusu hali ya utata iliyojitokeza kufuatia uvujaji  wa Mkataba wa Nyongeza wa Statoil kwa manufaa ya taifa.  

TUNAELEWAkwamba uziduaji wa rasilimali unajumuisha maamuzi  magumu yenye mwingiliano  mkubwa, makubaliano ya kibiashara yenye maslahi kwa pande zote na masharti ya muda mrefu. Haya maamuzi  yatakuwa ya kuaminika zaidi na hayatakiukwa kwa urahisi  ikiwa wananchi wanaelewa sababu za kiuchumi zilizofanya maamuzi hayo kuchukuliwa. Jambo la msingi hata hivyo, ni kwamba sera za kifedha  na masharti ya mikataba ni budi yazingatie kuwa nchi inanufaika ipasavyo kutokana na rasilimali, pamoja na kuvutia uwekezaji unaohitajika ili kupata manufaa yanayotakiwa.  Serikali na wawekezaji kwa kawaida hupata huduma bora zaidi  iwapo kuna kanuni  / sheria za wazi  zinazofuatwa na wawekezaji wote kwa mazingira yanayofanana. Uwazi na sheria / kanuni zinazofanana husaidia kufanya watendaji  kufahamu kuwa huduma  hazibagui, hupunguza fursa za rushwa na huweza kupunguza madai  kutoka kwa wawekezaji mmoja moja  kupewa upendeleo fulani .

TUNASISITIZA  haki ya uwajibikaji kijamii kwa maana kwamba wananchi wana haki ya msingi kupata maelezo na uthibitisho toka kwa watendaji waliopewa wajibu wa kusimamia mali asili zao.   Kwa upande mwingine, watendaji nao wanapaswa kutoa uthibitisho kuhusu maamuzi wanayofanya katika utumiaji wa hizi rasilimali.

TUNASIKITISHWA  na ufinyu wa taarifa zinazotolewa kwa umma  hali inayopelekea katika uharibifu na hali ya hatari  na ya kukanganya kuhusu mikataba ya gesi asilia na viwanda vya uziduaji  kwa ujumla. Uvujaji wa taarifa za  Mkataba wa Nyongeza wa Ushirikiano katika Uzalishaji (PSA) uliopo kati ya Serikali na Statoil unaibua  masuala haya:

·         Mwitikio mdogo kutoka kwa Serikali na kutokuwepo mwitikio kabisa kutoka Statoil kunaleta hali ya kutokuwa na uhakika na ya mashaka. Mwitikio wa serikali  kwa kupitia tamko kwa vyombo vya habari lililotolewa na TPDC kwa ujumla linadai kuwa masharti  ya PSA hiyo ni  mazuri  kwa nchi  kwa kunukuu 61% zinazoingia serikalini. Tamko  liliendelea kutuhumu vyombo vya habari kwa kutokuwa na taarifa  wakati huo huo likitoa  maelezo yasiyo sahihi kwamba  bila Statoil kutia sahihi PSA mwaka 2007, ujazo wa futi  trilioni 50. 5 usigegundulika, kwa hiyo kudhania kuwa ugunduzi wote unatokana na Statoil! Hili linaibua swali zaidi kama tofauti iliyopo ni malipo ya ziada (bonasi) kwa Statoil kwa ajili hiyo? Tamko halitoi taarifa zozote kuhusu sababu za msingi za kiuchumi  na matarajio  yaliyotegemewa kuthibitisha tofauti  kutoka Mkataba wa Nyongeza wa Mfano na  PSA wala masharti halisi ya mkataba wa PSA uliotiwa sahihi.  

·         Ukimya mkubwa wa Statoil kuhusu suala ambalo linatishia siyo tu sifa yake kama kampuni bali na ya nchi yake (Norway) iliyo mstari wa mbele katika uwazi wa viwanda vya uziduaji.

·         Mmomonyoko unaoendelea wa imani ya umma kuhusu jinsi sekta ya uziduaji inavyosimamiwa kwa kuchota uzoefu unaotisha wa sekta ya uchimbaji madini. Ikiwa umma utaaminishwa kuwa mkataba wa serikali na Statoil ulikuwa mzuri  kutegemea  taarifa walizokuwa nazo  wakati wa kutiliana sahihi kwenye Mkataba wa Nyongeza, taarifa zote husika lazima ziwekwe wazi.

·         Usiri unaoendelea kuhusu suala hili  ambalo sasa  hivi linajadiliwa na umma unaongezea hali ya wananchi kutokuwaamini hao waliopewa jukumu la kusimamia rasilimali. Uchambuzi wa hivi karibuni wa Taasisi ya Usimamizi wa Mali Asili (The Natural Resource Governance Institute - NRGI) unaonyesha kuwa inawezekana kuwa ni mapema mno kuwa na uhakika kama Tanzania ilipata au haikupata kiwango kikubwa kutokana na  Mkataba wa Nyongeza wa Statoil wa mwaka 2012 kwa kuzingatia kuwa Mkataba wa awali wa PSA wa mwaka 2007 na taarifa nyingine zilizowezesha mahesabu ya serikali bado  hazipatikani kwa umma.                                                                                                                                                         

·         Namna ambavyo Mkataba wa Nyongeza wa  Statoil uliletwa na kuanza kujadiliwa na umma  (kwa kuvuja)  inashusha hadhi ya serikali kwani inaleta mashaka mengi na inaweza kufanya wengine kudhani kuwa lengo lilikuwa kufichua rushwa katika makubaliano hayo.  Uvujaji huo  unawasukuma wadau wote: viwanda, serikali na jumuiya za kiraia kuanza mazungumzo  ya dhati kuhusu usiri unaoendelea katika mikataba ya viwanda vya uziduaji ingawa manufaa ya kuweka mambo wazi yanaonekana waziwazi.

·         Kuzuia suala muhimu la umma kujadiliwa kwa taarifa nusunusu za kuvuja, wadau sharti waanze majadiliano  ya kweli na  ya wazi kuhusu uhalali wa   kisheria wa  serikali na viwanda vya uziduaji  kukataa mara nyingi kuweka wazi mikataba  hiyo.

·         Ieleweke pia kuwa uwazi wa mikataba ni sharti moja kwa makampuni (e.g. mfano Swala kupitia sharia za Mamlaka ya Masoko ya Dhamana na Mitaji) na itakuwa lazima kwa mikataba ya uziduaji  itayotiwa sahihi baada ya 2014 kama serikali ijayo itadumisha dhamira chini ya Mpango Kazi wa Mpango wa Uendeshaji Shughuli za Serikali kwa Uwazi (Open Government Partnership Action Plan). Tunauliza kwa nini kampuni zingine zishinikizwe kuwa wazi wakati zingine hazilazimishwi?

·         Jumuiya za kiraia, wabunge na wananchi wamekuwa wakitoa hoja za kutaka bunge lipitishe mikataba ya uziduaji baada ya rasimu za mikataba hiyo kuandaliwa na kujadiliwa na serikali. Upitishwaji wa Mkataba wa Statoil (PSA), Mkataba wa Nyongeza na Mikataba mingine kama hiyo na Bunge kungehakikisha  kuwa wawakilishi wa wananchi  wamepata muda wa kutosha kujadili ubora wa mikataba hiyo kabla haijaanza kutekelezwa  na ni njia nyingine ya kuleta mikataba hiyo mbele ya umma.  Pia inazuia makampuni kuhamisha rasilimali kwenda nje ya nchi kimagendo. Serikali inaweza kusita kuhusu mkataba wa Statoil kuwekwa wazi kwa umma kwa maana kutaweza kuthibitisha kwa umma kuwa Mkataba wa Nyongeza wa Statoil PSA  ulikuwa  kweli hauna maslahi mazuri na hivyo kuibua madai  ya kuujadili mkataba huo upya (renegotiation). Hili  siyo lazima liwe  na madhara kwa serikali wala kwa makampuni. Kutokana na mabadiliko katika hali ya kiuchumi, ni kawaida kwa mikataba ya uziduaji kujadiliwa upya bila kuvuja kwake. Kuingia mkataba mpya kunaweza kusaidia kurudisha imani kwa wananchi na kusaidia shughuli za uziduaji kufanyika kwa tija kwa mtazamo wa muda mrefu.

·         Mjadala  mrefu wa umma kuhusu Mkataba wa Nyongeza wa Statoil (PSA) unaonesha uelewa tofauti juu ya mikataba ya uziduaji. Uelewa mdogo wa nini kiko ndani ya mikataba hii unazuia juhudi za kuweka uwazi katika sekta ya uziduaji.   

Kutokana  na yaliyotajwa hapo juu, TUNATAKA Serikali:

·         Iweke wazi kwa umma Mkataba uliotiwa sahihi (nakala halisi) wa Statoil (PSA) wa mwaka 2007 kwa uchambuzi wa umma.

·         Iweke wazi  kwa umma mikataba yote 25 ( PSAs) iliyowekwa sahihi pamoja na mipya itakayotiwa sahihi kwa lengo la kutoa haki sawa kwa wadau wote katika viwanda.

·         Ianzishe utaratibu wa bunge kuridhia  mikataba yote ya uziduaji baada ya kujadiliwa na kutiwa sahihi na Waziri husika.

·         Jamii, vyombo vya habari na serikali  budi zitoe kipaumbele  katika kuhakikisha kuwa uwezo wa wadau wao kuingia katika mijadala ya uziduaji unaimarishwa

Zaidi  ya hayo,TUNATAKA: 

·         Statoil itoe maelezo kwa umma kuhusu sababu zilizowasukuma (kama zipo) za kutenda tofauti  na Mkataba wa Mfano  (Model PSA)

·         Makampuni yote ya Mafuta, Gesi na uchimbaji madini yanayoendesha shughuli zao Tanzania  na serikali kufanyia mapitio vipengele vyote vya usiri katika mikataba ya uziduaji  kwa manufaa ya umma  na yaache kuingiza vipengele kama hivyo katika mikataba mipya.

TUNAPENDEKEZA yafuatayo ili kufanyia kazi suala zima la usimamizi  wa uziduaji:

·         Kuunda Sheria ya Uhuru wa Habari

·         Kuanzisha hifadhi ya mikataba  kwa kutumia kompyuta (database)  

·         Makampuni ya Uziduaji yafanyie mapitio sera zao za usiri.

Wadau:

1.            Interfaith Standing Committee on Economic Justice and the Integrity of Creation

2.            HakiMadini

3.            Policy Forum

4.            Oil and Natural Gas Environment Alliance (ONGEA)