Skip to main content
Submitted by Web Master on 28 April 2009

Bajeti kwa kawaida imekuwa ikichukuliwa kuwa ni kazi ya wataalamu, wachumi na wahasibu tu. Lakini uamuzi wa Serikali wa namna gani ya kukusanya mapato huwaathiri wananchi wote. Kiwango cha Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) na kodi nyingine huathiri bei za vitu vinavyotumiwa katika kaya. Uamuzi wa matumizi ya serikali ndio huweka wazi iwapo viwango vya mishahara ya walimuna iwapo kutakuwa na dawa na vifaa vya kutosha katika zahanati au la.

Wakati huo huo, bajeti hutupatia pia nafasi ya kuelewa msukumo ‘halisi’ wa kisera wa serikali katika ngazi ya taifa na wilaya. Sera zisizokuwa na rasilimali za kuzitekelezea hubakia kuwa katika makaratasi tu.

Kimsingi, bajeti inahusiana na pesa za wananchi. Kwa bahati mbaya, mchakato wa kuamua namna ya kuzitumia hizo pesa na namna ya kusimamia kuhakikisha kuwa zinaenda zinakotakiwa kwenda ni mgumu kwa wananchi wa kawaida kuweza kushiriki. Sehemu kubwa ya taarifa zinazohusiana huwa haziwekwi wazi kwa umma, na hata zile zinazopatikana huwa katika namna iliyongumu kueleweka. Hivyo, wananchi wengi huwa hawana fursa ya kushiriki katika michakato ya bajeti. Kwa ujumla, michakato mingi rasmi huwa haiku wazi kwa
wananchi.

Shirika la HakiElimu, kwa kushirikiana na Kikundi kazi cha Bajeti (Budget Working Group (BWG)) cha mtandao wa Asasi Zisizo za Kiserikali (AZISE) wa Policy Forum, limeandaa muongozo huu katika jitihada za kuziba pengo hilo la uelewa wa wananchi na kuwawezesha kushiriki kikamilifu zaidi katika mchakato huu.

Muongozo huu umejengwa kwenye jitihada za Kikundi kazi hicho za kuirahisisha bajeti kila mwaka na kufanya uchambuzi wa bajeti hizo kupitia mtiririko wa mihutasari ya kibajeti. Tunaamini kuwa ushiriki mkubwa zaidi wa umma na uchunguzaji wa bajeti utaboresha uwajibikaji na kuziba mianya zaidi ya ufisadi.

Tunaamini kuwa mwongozo huu utafanyika kuwa msaada kwa Wabunge na wawakilishi wa ngazi nyingine za chini katika kuijadili bajeti, waandishi wa Habari wanaoandika Habari za bajeti, Asasi za Kiraia (AZAKI) zinazopenda kujishughulisha na masuala ya bajeti pamoja na wananchi wote kwa ujumla.

Muongozo unaanza kwa mapitio ya mchakato wa bajeti. Tunawajadili wahusika wakuu na hatua za muhimu katika michakato ya bajeti kitaifa na katika ngazi za chini. Katika Sehemu ya II tunaingia kwa kina zaidi na kuonesha ‘picha halisi’ ya muundo wa kisera na kisheria katika uandaaji na utekelezaji wa bajeti, pamoja na taarifa zaidi kwa ajili ya kuelewa na kutaathimini sehemu kuu mbili za bajeti –
mapato na matumizi. Sehemu ya III inajadili maoni mbadala kuhusiana na bajeti na mchakato wake nchini Tanzania, na kutoa mapendekezo kwa ajili ya maboresho. Mwisho, imetolewa orodha ya rejea za muhimu pamoja na faharasa
ya istilahi za kibajeti.

Tunalenga zaidi katika nadharia, (namna mambo yanavyopaswa kufanyika) lakini pia tunajadili namna mchakato wa bajeti unavyofanyika kivitendo na kuingiza baadhi ya taarifa za hivi karibuni za bajeti. Muongozo huu utatolewa kwa lugha
rahisi mwaka 2009.

Mwisho, ni muhimu kutaja kwamba mchakato wa bajeti ni mgumu, na kuelewa namna unavyofanya kazi linaweza kuwa ni suala la majadiliano. Tumekuwa makini katika kutaja rejea zote zilizotumika na kuangalia kwa makini usahihi wa taarifa zote pamoja wataalamu. Hata hivyo, inawezekana baadhi ya taarifa zilizoko katika muongozo huu zimepitwa na wakati au haziko sahihi. Wasomaji wanaombwa kuwasiliana nasi kuhusiana na makosa yoyote ili tuweze kuyashughilikia katika matoleo yajayo.

Attachment Size
PFKUUELEWAMCHAKATOFINAL.pdf 1.9 MB