Wakati Waziri wa Fedha anapowasilisha Bajeti ya Taifa kwa mwaka wa Fedha 2014/15 Bungeni kesho, sisi Wajumbe wa Kikundi Kazi cha Bajeti cha Policy Forum, tunaowakilisha zaidi ya Asasi 70 za Kiraia tuliounganisha nguvu zetu ili kuongeza uelewa na ushiriki wa jamii katika uandaaji wa sera, tunapenda kutoa mchango wetu katika mchakato huu muhimu.
Bajeti hii ya Taifa inawasilishwa baada ya mwaka wa fedha uliokuwa mgumu ulioshuhudia upungufu wa mapato kwa mwaka 2013/14 ikiwa na maana kwamba matumizi yaliyopangwa yalizidi bajeti iliyopitishwa, hali ambayo iliathiri miradi ya miundo mbinu na huduma za kijamii, ikipunguza pia mchango wa Serikali kwa sekta za afya na maji, pia kulikuwa na ucheleweshaji katika upelekaji wa fedha za serikali na za wabia wengine wa maendeleo kwa mwaka wa fedha 2013/14. Tukizingatia masuala haya nyeti, tunaleta mapendekezo yetu muhimu ya kisera kama ifuatavyo:
Ukusanyaji wa Rasilimali (Mapato) za Ndani
Kabla ya kuwasilishwa kwa Bajeti ya Taifa ya mwaka 2012/13 miaka miwili iliyopita, Kikundi Kazi cha Bajeti cha Policy Forum kiliona kwamba Tanzania ina uwezo wa kukusanya kodi kufikia kiwango cha 20.9% ya Zao Ghafi la Ndani (GDP), kulingana na makadirio ya Mfuko wa Kimataifa wa Fedha (IMF) lakini imekuwa ikikusanya kiasi kinachozidi kidogo 14% (kwa makadirio ya 2009/10). Ingawa mapato ya kodi kama sehemu ya Zao Ghafi la Ndani (GDP) yamekuwa yakiongezeka taratibu (15.2% kwa mwaka 2010/11 na yanategemewa kufikia 16.2% kwa mwaka 2013/14), hii bado ni pungufu ya uwezo uliopo uliothibitishwa. Sheria ya mabadiliko ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) itakayoanza kutumika hivi karibuni izingatie suala la upunguzaji wa misamaha ya kodi ambazo zinafikiriwa kimakosa kuvutia na kudumisha Uwekezaji wa Nje ndani ya nchi wakati zinasababisha upotevu mkubwa wa mapato. Tunapongeza serikali kwa kuonesha nia ya kupunguza changamoto za upotevu wa mapato na kuanzishwa kwa sheria ya mabadiliko ya kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kunadhihirisha nia hii. Hata hivyo, Policy Forum inaona kwamba, nguvu zaidi zielekezwe katika kufikia lengo la serikali la kupunguza kiwango cha misamaha ya kodi ikilinganishwa na Zao Ghafi la Ndani (GDP) hadi 1.2%. Kiwango cha sasa hivi ni 4.3% ya Zao Ghafi la Ndani.
Afya
Bajeti ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii inatarajiwa kupunguzwa kwa kiwango cha 17.4% toka shilingi za Tanzania 754 billioni kwa mwaka 2013/14 hadi shilingi 623 billioni kwa mwaka 2014/15. Sababu kuu ya upungufu huu ni mchango mdogo zaidi toka kwa Wabia wa Maendeleo ambao utapunguzwa kwa kiasi cha shilingi za Tanzania bilioni 182. Hali hii itaathiri zaidi upatikanaji wa fedha kwa ajili madawa muhimu na vifaa vya matibabu . Wakati misaada toka nje inakatwa kwa kiwango cha bilioni 17.7, Serikali inasita kuziba pengo lililopo ambalo sasa linazidi shilingi za Tanzania bilioni 200.
Ikiwa Bunge litapitisha bajeti hii kama ilivyowasilishwa, itasababisha kuisha kila mara kwa madawa muhimu katika vituo vya afya vya serikali katika mwaka ujao wa fedha. Katika muktadha wa Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiuchumi, Kijamii na Kitamaduni ambayo serikali ya Tanzania iliridhia mwaka 1976, serikali inashindwa kwa kiasi kikubwa katika wajibu wake wa kuhakikisha kuwa kila mtu anafikia huduma ya matibabu ambayo inajumuisha uwepo wa madawa muhimu kwa wananchi ambao hawana uwezo wa kugharimia madawa hayo.
Pia kuna masuala ya uwajibikaji ambayo yanahitaji uchunguzi wa kina. Baada ya kutolewa kwa maoni rasmi ya kiukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu (CAG) , Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii inahitaji kuboresha mtiririko wa taarifa zake za ukaguzi na kuamua kuchukua hatua. Inapaswa kuimarisha Kitengo chake cha ukaguzi wa ndani na kufanya kazi kwa karibu na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu (CAG) pamoja na Bunge kufanya marekebisho stahiki ili kuzuia hoja nzito zingine za kiukaguzi . Ikiwa na maoni safi ya kiukaguzi, Wizara itakuwa katika nafasi nzuri zaidi kupata msaada wa kisiasa na wa kifedha kwa changamoto zinazokuja siku za mbeleni.
Elimu
Bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imeongezeka kutoka shilingi za Tanzania bilioni 689.7 kwa mwaka 2013/2014 hadi shilingi 794 bilioni kwa mwaka 2014/15. Cha kuvutia, Bajeti ya Maendeleo ya Wizara imeongezeka toka shilingi bilioni 72 kwa mwaka 2013/14 hadi shilingi bilioni 454 mwaka 2014/15. Kuhusu matumizi ya kawaida, yamepungua toka shilingi bilioni 612 mwaka uliopita hadi shilingi bilioni 340 mwaka 2014/15.
Pamoja na hayo, hizi takwimu zilizopitishwa zinazua masuala mbalimbali mbele yetu. Ingawaje bajeti inaonekana imeongezeka kitakwimu, bajeti ya Maendeleo ya Wizara imepunguzwa. Hii ni kwa sababu kiasi kidogo kilichoongezeka mwaka huu kimetokana na mpangilio mpya wa kifungu cha 7001 kutoka Elimu ya Juu - 270900 ambacho mwaka 2013/14 kiliwekwa kama bajeti ya kawaida cha kifungu cha 1003 (Sera na Mipango) ambacho kiko chini ya matumizi ya Maendeleo kwa mwaka 2014/15.
Hii inamaanisha kuwa sehemu kubwa ya kinachoitwa bajeti ya maendeleo haitumiki kweli kama bajeti halisi ya maendeleo bali inaelekezwa kwenye Elimu ya Juu kama mikopo kwa wanachuo kwa matumizi yao ya kawaida. Suala la kama mikopo ya wanachuo ichukuliwe kama uwekezaji linahitaji mjadala kwa sababu mikopo hiyo haina faida na urejeshaji umekuwa ni changamoto. Kwa hiyo ukiangalia takwimu kwa makini, utaona kuwa Wizara bado inatumia fedha kidogo katika miradi ya elimu. Hii ni kweli kwa kuwa kati ya shilingi bilioni 454 iliyopangwa kwa matumizi ya maendeleo, shilingi bilioni 307 zimepangwa kwa Bodi ya Mikopo ya Wanachuo wa Elimu ya Juu kwa ajili ya mikopo ya wanachuo. Hii ni 68% ya jumla ya bajeti ya Maendeleo ya Wizara.
Kilimo
Sekta ya Kilimo ni mojawapo ya sekta muhimu Tanzania kwa sababu kadhaa. Kati ya hizo ni pamoja na ukweli kwamba sekta hii inaajiri zaidi ya nusu ya wakazi wa Tanzania (74%) na ilichangia 24.8% kwa mwaka 2012 na 24.7% kwa mwaka 2013 ya Zao Ghafi la Ndani (GDP).
Pamoja na huu wajibu muhimu ambao sekta hii inayo katika uchumi, inakumbana na changamoto kadhaa kuanzia ndani hadi nje ya sekta. Ndani ya sekta, kuna uthibitisho wa matumizi mabaya ya fedha za umma zilizopangiwa sekta hii, na kutokana na hili miradi ya maendeleo imeshindwa kutekelezwa vizuri. Nje ya sekta, utoaji wa fedha kwa sekta hii haujawa mzuri. Kumekuwa na ucheleweshaji wa upelekaji wa fedha ambao umethibitishwa pamoja na uwasilishaji wa fedha zisizotosheleza.
Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu (CAG) kwa mwaka 2012 inaonesha kuwa miongoni mwa makosa ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika iliyopelekea Wizara kupewa hati isiyoridhisha na CAG ni ukosefu wa nyaraka za kuthibitisha matumizi ya kiasi cha shilingi 2, 162,343,978. Tunahimiza Wizara izingatie mapendekezo ya CAG ili kuboresha nidhamu ya fedha.
Kwa upande wa utoaji, ucheleweshaji umekuwa kawaida. Wakati haifiki hata miezi mitatu hadi mwaka wa fedha 2013/14 kuisha, hadi 31 Machi, 2014, Hazina ilikuwa imetoa 50.4% tu ya bajeti ya maendeleo ya Sekta ya Kilimo.
Kinachofurahisha kuhusu bajeti ya mwaka huu ya Kilimo ni ongezeko la uwajibikaji wa serikali kutoa fedha za kuendesha miradi ya maendeleo. Hili ni jambo la kupongezwa, lakini inabakia changamoto kama serikali itaweza kweli kupata kiasi hicho cha fedha na kuzipeleka kwa miradi iliyopangwa. Kwa mfano, kwa mwaka 2013/14 serikali ilipanga kukusanya shilingi bilioni 3.2 lakini hadi Machi 31, 2014 iliweza kukusanya shilingi bilioni 1.7 (53.7%) tu.
Pamoja na kwamba tunaipongeza Serikali kwa ahadi yake ya kutoa fedha kwa sehemu kubwa ya miradi yake ya maendeleo, ni wakati sasa wa makusanyo ya mapato kuboreshwa ili kuendana na dhamira hiyo. Zaidi ya hayo, bajeti ya kilimo bado iko mbali kufikia lengo la Azimio la Maputo la mwaka 2003 kuhusu Kilimo na Chakula inayosema kwamba walau 10% ya Bajeti yote ya Taifa ipangiwe sekta ya Kilimo.
Maji
Programu ya Sekta ya Maendeleo ya Maji (WSDP) iliyozinduliwa mwaka 2006 ilionesha kuwa ni moja kati ya mbinu pana za Kisekta katika Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara. Imevutia ahadi zinazofikia Dola za Marekani bilioni 1.7 kwa kipindi cha April 2014. Fedha zimeelekezwa katika Menejimenti ya Rasilimali Maji, Usambazaji Maji Vijijini, Usambazaji Maji Mijini, na Menejimenti ya Rasilimali Maji, Upatikanaji wa Maji Vijijini, Upatikanaji wa Maji Mijini, na Ujenzi wa Uwezo wa Kitaasisi.
Kwa ujumla sekta imeshuhudia ongezeko katika utoaji wa fedha hasa katika kitengo cha vijijini kati ya mwaka 2012/13 na 2013/14. Kwa mara ya kwanza, tumeshuhudia ongezeko kubwa la kipengele cha bajeti ya vijijini toka shilingi 120,787,537,924 mwaka 2012/13 hadi shilingi 345,805,362,000 mwaka 2013/14. Hili linastahili pongezi.
Licha ya ongezeko la fedha zilizopitishwa kwa ajili ya sekta, awamu ya kwanza ya mpango ilikabiliana na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na uchelewaji katika utoaji wa fedha toka serikalini na pia toka kwa Wabia wa Maendeleo kwa mwaka 2013/14. Jambo lingine linaloleta mashaka ni kwamba sekta ya maji bado ni tegemezi kwa hisani ya wafadhili, hilo linazua maswali kuhusu uendelevu wa miradi ya maji kote Tanzania.
Licha ya changamoto za utoaji, uchunguzi wa kile kidogo kinachotolewa unaibua maswali kama tunapata thamani ya fedha kama ilivyokusudiwa. Mapitio ya Mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP I) ulionesha ukosefu wa kijumla wa ukaguzi wa kiufundi ili kufahamu kama fedha zilizotolewa zinatumika ipasavyo na kama taratibu za manunuzi zimefuatwa. Kwa kigezo cha utendaji kazi wa matoleo ya maji (water point) ya 54% tutawezaje kuhakikisha kuwa maji yanatumika ipasavyo?
Wakati mwaka mpya wa fedha unakaribia kuanza, tunatoa wito wa kufanyika kwa Mapitio ya sekta ili kuboresha uendelevu wa matoleo ya maji na upatikanaji wa fedha.
Jinsia
Masuala ya maji, kilimo, afya na elimu yote yana uhusiano mkubwa na Wanawake . Nchini Tanzania, 98% ya wanawake wa vijijini walio na nguvu za kufanya kazi wanajishughulisha na kilimo na wanazalisha kiwango kikubwa cha mazao ya chakula kwa matumizi ya kaya na pia kwa mauzo nje ya nchi. Kwa hiyo ingelifaa ionekane dhahiri kuwa bajeti ya kilimo inazingatia suala la usawa wa jinsia, kwa mfano zitengwe fedha kiasi fulani kwa ajili ya kupanua wigo wa wanawake kufikia huduma rasmi za kifedha ili kuimarisha miradi yao ya kilimo, pia kuwezesha wanawake wakulima kufikiwa na huduma za ugani. Hali kadhalika, uingizwaji wa masuala ya jinsia kunapaswa kudhihirika katika sekta za elimu, afya na maji ili maisha ya wanawake yaboreke.
Vipaumbele vingi vya bajeti ya mwaka 2014/15 vinahusu uwekezaji katika miradi mikubwa ambayo kwa sehemu kubwa inamilikiwa na wanaume na ina matarajio ya matokeo ya muda mrefu kwa wakulima kama vile miradi ya umwagiliaji maji na kilimo cha mashamba makubwa. Hata hivyo, masuala ya pembejeo kama vile mbegu bora au upatikanaji wa fedha vijijini (mikopo) ambayo yanaweza kuleta matokeo yanayofanana na hayo lakini kwa kutumia rasilimali ndogo zaidi hayaonekani kutiliwa mkazo.
Hitimisho
Kwa uelewa kwamba miradi yetu mingi ni tegemezi kwa wafadhili wa nje, tunahimiza serikali kupanua wigo wake wa kodi kutuwezesha kukusanya rasilimali za kutosha kuendesha miradi yetu mbalimbali ya maendeleo. Hili ni jambo muhimu sana hasa katika muktadha wa upunguzwaji wa fedha kutoka kwa wafadhili .
Wakati serikali inaanza hatua za kukusanya rasilimali, ni muhimu pia uwajibikaji kwa upande wa matumizi ya rasilimali kuimarishwa. Sambamba na hili ni uboreshaji wa uwazi katika matumizi ya fedha zinazotumika katika utoaji wa huduma za umma.
Masuala ya kisera tuliyozungumza hapa yanahitaji kujitoa kwa kiwango kikubwa ili kuyatekeleza. Mifumo ya maji, afya na elimu pamoja na sekta ya kilimo haiwezi kuachwa kuendelea kushindwa. Jamii yenye lishe nzuri, iliyoelimika na yenye stadi ni muhimu kwa ukuaji wa uchumi wa nchi. Kwa sababu hii, tunahimiza serikali itilie maanani haya mapendekezo machache, tunapofanya kazi pamoja katika kuzifanya sera zitende kazi kwa watu wa Tanzania.